Habari za UN - Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu United Nations
-
- News
Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu
-
Watoa chanjo wavuka mabonde na mito kufikisha chanjo kwa walengwa Tanzania
Wiki ya kimataifa ya chanjo ikifungua pazia, nchini Tanzania wahudumu wa afya kama Prisca Mkungwa wanajitoa kwa kadri ya uwezo wao kuhakikisha huduma za chanjo zinafikia walengwa wote hata wale walioko maeneo ya mbali. Mathalani huko wilayani Chunya, mkoani Mbeya, kusini magharibi mwa taifa hilo ambako kupitia ushirikiano na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF, chanjo dhidi ya surua inatolewa kwa watoto. Prisca na wenzake kutokana na kupenda kazi yao wanafanya kila njia iwe ni kutumia usafiri wa bodaboda au hata kuvuka mito na mabonde kwa miguu kuhakikisha chanjo zinafika. Kufahamu kwa kina ungana na Assumpta Massoi katika makala hii iliyoandaliwa na UNICEF Tanzania.
-
Wiki ya Chanjo Duniani yaanza leo 24 hadi 30 Aprili
Leo ni siku ya kwanza ya siku saba za Wiki ya Chanjo Duniani.
(Taarifa ya Anold Kayanda)
Wiki ya Chanjo Duniani ambayo huadhimishwa katika kila wiki ya mwisho ya mwezi Aprili, inalenga kuangazia hatua za pamoja zinazohitajika na kuhimiza matumizi ya chanjo kuwalinda watu wa rika zote duniani dhidi ya magonjwa.
Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni, WHO linashirikiana na nchi kote ulimwenguni kuhamasisha ufahamu wa thamani ya chanjo na uchanjaji na kuhakikisha kuwa serikali zinapata mwongozo unaohitajika na usaidizi wa kiufundi ili kutekeleza programu za uchanjaji zenye ubora wa hali ya juu.
Lengo kuu la Wiki ya Chanjo Duniani ni kwa watu zaidi na jamii zao kulindwa dhidi ya magonjwa yanayoweza kuzuilika.
WHO inasema chanjo zimesaidia sana ikitolea mfano namna ulimwengu umeweza kutokomeza ugonjwa wa ndui ambapo mtu wa mwisho kuugua ugonjwa huo ni miaka 47 iliyopita.
Mwaka huu Wiki ya Chanjo Duniani inaadhimisha miaka 50 ya EPI ambao ni mpango ambao WHO iliuanzisha mwaka 1974 kwa lengo la kufanya chanjo zipatikane kwa watoto wote duniani.
WHO inatoa wito kwa nchi kote duniani kuongeza uwekezaji katika mipango ya chanjo ili kulinda vizazi vijavyo.
Tags: Siku za UN, WHO, Chanjo, EPI, Wiki ya Chanjo Duniani -
Mtu 1 kati ya 5 katika nchi 59 duniani anahitaji hatua za haraka kuepushwa na baa la njaa: FAO
Ripoti mpya ya kimataifa iliyotolewa leo na shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO kuhusu mgogoro wa chakula duniani inasema karibu watu milioni 282 walio katika nchi 59 walikabiliwa na viwango vya juu vya njaa mwaka 2023.
(TAARIFA YA FLORA NDUCHA)
Asante Leah. Kwa hakika ripoti hiyo ya “Mgogoro wa kimataifa wa chakula” GRFC inasema kiwango cha watu wenye njaa duniani kiliongezeka kwa watu milioni 24 kutoka mwaka 2022 hadi 2023 na ni asilimia 21.5 ya watu waliofanyiwa tahimini na hicho ni kiwango kikubwa sana ukilinganisha na ilivyokuwa kabla ya janga la COVID-19 limesema shirika la FAO likiongeza kuwa idadi ya walio na njaa duniani inaendelea kuongezeka.
Ripoti imetaja sababu kuu tatu ambazo zinachangia kwa kiasi kikubwa janga la njaa duniani ambazo ni mosi migogoro na vita ambapo inasema inaathiri katika nchi 20 zilizo na jumla ya watu milioni 135 wanaokabiliwa na njaa zikiwemo Sudan, Yemen na Palestina katika Ukanda wa Gaza.
Pili ni matukio mabaya ya hali ya hewa yaliyochangiwa na mabadiliko ya tabianchi ambayo yamekuwa chanzo cha njaa katika nchi 18 na kuathiri kwa njaa zaidi ya watu milioni 77.
Na tatu mdororo wa kiuchumi uliokuwa chachu ya njaa katika nchi 21 na kuathiri jumlaya watu milioni 75.
FAO imesema kwa miaka minne mfululizo takriban asilimia 22 ya watu waliofanyiwa tathimini duniani wamekuwa wakikabiliwa na kutakuwa na uhakika wa chakula. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema “Mgogoro huu unahitaji hatua za haraka. Kutumia takwimu zilizoainishwa katika ripoti hii ili kufanyia marekebisho mifumo ya chakula na kushughulikia mizizi ya kutakuwa na uhakika wa chakula itakuwa muhimu sana”
Kwa mujibu wa ripoti waathirika wakubwa ni watoto, wanawake na watu wenye ulemavu.Mtandao wa kimataifa dhidi ya mgogoro wa chakula imetoa wito wa haraka wa kubadili mtazamo ili ujumuishe amani, hatua za kuzuia na za maendeleo sambaba na juhudi za dharura kuvunja mzunguko wa janga la njaa ambalo linasalia katika viwango vya juu
-
24 APRILI 2024
Karibu kusikiliza jarida hii leo linaangazia masuala mbalimbali ikiwemo ripotoi ya mgogoro wa chakula duniani, kuanza kwa wiki ya chanjo na utoaji chanjo kwa watoto mashinani.
-
23 APRILI 2024
Hii leo jaridani utasikia kuhusu ushirikishwaji wa vijana katika vita dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kutoka shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa Maendeleo UNDP.
Pia utasikia muhtasari wa habari kuhusu wasaka hifadhi huko nchini Uingereza kuhamishiwa Rwanda, Makaburi ya halaiki huko Gaza na kuongezeka kwa mlipuko wa ugonjwa wakipindi pindu duniani.
Kwa upande wa mashinani hii leo utasikia kuhusu harakati za mashirika ya Umoja wa Mataifa na serikali katika kuhakikisha usalama wa mipaka. -
Rein Paulsen: Wakati wa kuchukua hatua kuepusha baa la njaa Sudan ni sasa
Katika mahojiano na Idhaa ya Umoja wa Mataifa, afisa mwandamizi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) anayehusika na masuala ya dharura na mnepo, Rein Paulsen ametahadharisha kuwa hatari ya kutokea baa la njaa nchini Sudan ni halisi na kwa hivyo wakati wa kuchukua hatua ni sasa. Sabrina Moshi anasimulia.