Habari za UN - Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu United Nations
-
- News
Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu
-
Jifunze Kiswahili - Pata ufafanuzi wa neno "Nyendea"
Katika kujifunza lugha ya Kiswahili leo Mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania, BAKITA anafafanua matumizi ya neno “NYENDEA”
-
06 JUNI 2024
Katika Jarida la habari za Umoja wa Mataifa hii leo Flora Nducha anakuletea
-Gaza Nuiserat Israel imeshambulia shule moja iliyokuwa inahifadhi wakimbizi 6,000 wa kipalestina na kuua watu 35, na wengine wengi wamejeruhiwa,
-Hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa leo kumefanyika tukio la kukumbuka wafanyakazi 188 wa chombo hicho waliouawa mwaka 2023 pekee wakiwemo 135 watumishi wa UNRWA waliouawa ukanda wa Gaza
-Duniani kote mtoto mmoja kati ya wanne anaishi katika mazingira ya umaskini wa chakula akila aina moja au mbili tu ya mlo kutokana na vita, mizozo, janga la tabianchi na ukosefu wa uwiano, imesema ripoti mpya iliyotolewa leo na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF.
-Katika mada kwa kina utamsikia Erick Mukiza mmoja wa wanasheria waliothibitishwa kuwa wapatanishi au wasuluhishi wa migogoro nje ya mahakama nchini Tanzania na mipango yake ya kujumuisha wenye ulemavu ili wanufaike na mpango huo wa serikali ya Tanzania.
-Na katika jifinze Kiswahili Onni Sigalla anafafanua maana ya neno Nyendea -
UN: Kila mtu ana wajibu wa kuhusika na urejeshaji wa ubora wa ardhi
Leo ni siku ya mazingira duniani na Umoja wa Mataifa unaisa dunia kuchukua hatua sasa kurejesha Uhai wa ardhi iliyoharibiwa na kujenga mnepo dhidi ya kuongezeka kwa hali ya jangwa na ukame na hiyo ndio kaulimbiu ya siku ya mwaka huu. Akisisitiza maudhui hayo Inger Andersen Mkurugenzi mtendaji wa shirika la mazingira la Umoja wa Mataifa UNEP amemtaka kila mtu kujiunga na harakati za kimataifa za kurejesha ardhi yenye afya na kujenga mnepo wa majanga mengine kama vile ukame na hali ya jangwa. Flora Nducha anatupasha zaidi katika makala hii..
-
Lengo la kudhibiti ongezeko la joto duniani kwenye nyuzijoto 1.5 linaning’inia - Katibu Mkuu
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres asubuhi ya leo saa za New York, Marekani kupitia Hotuba Maalumu kuhusu Hatua Dhidi ya Mabadiliko ya Tabianchi ametahadharisha kuhusu hatari ya wazi ya uwezekano wa ongezeko la joto juu ya nyuzijoto 1.5 za selsiasi linaloukabili ulimwengu ikiwa uzalishalishaji wa hewa chafuzi utaendelea kwa viwango vya sasa. Assumpta Massoi na maelezo zaidi.
Ni hotuba ambayo imepewa jina “Wakati wa Ukweli”…Hotuba ambayo Katibu Mkuu wa Guterres ameitumia kuuleza ulimwengu ukweli kuwa utafiti wa kitaalamu unaonesha kuwa ni tani bilioni 200 tu za hewa ukaa ambazo dunia inaweza kuzihimili kabla ya kuvuka nyuzijoto 1.5 za Selsiasi juu ya viwango vya kabla ya viwanda jambo ambalo ni hatari kubwa kwa ulimwengu.
Ikumbukwe kuwa chini ya Mkataba wa Paris mnamo mwaka 2015, nchi zilikubaliana kupunguza kwa kiasi kikubwa uzalishaji wa hewa chafuzi duniani ili kuwezesha ongezeko la muda mrefu la wastani wa joto la uso wa dunia kuwekwa chini ya nyuzijoto 2 za selsiasi juu ya viwango vya kabla ya kuanza kwa viwanda na kuendeleza juhudi za kulipunguza joto hadi nyuzijoto 1.5 za selsiasi kisha kuhakikisha halizidi hapo.
Lakini kiongozi huyu wa Umoja wa Mataifa anaeleza kwamba kwa kasi ya sasa ya uzalishaji hewa chafuzi kwa kiasi cha tani bilioni 40 kwa mwaka ni wazi uwezo wa dunia kuendelea kudhibiti joto lisipande utaisha mapema.
“Sote tunaweza kufanya hisabati. Kwa kiwango hiki, uwezo wote wa dunia kuhimili hewa ukaa utaondolewa kabla ya mwaka 2030. Ukweli ni kwamba uzalishaji wa hewa chafuzi duniani unahitaji kushuka kwa asilimia tisa kila mwaka hadi mwaka 2030 ili kuweka hai kikomo cha ongezeko la nyuzi joto 1.5. Lakini zinaelekea kubaya. Mwaka jana zilipanda kwa asilimia moja. Ukweli ni kwamba tayari tunakabiliwa na mashambulizi katika eneo la nyuzijoto 1.5 za Selsiasi.” Amesema Guterres.
Guterres ameeleza kwamba hakuna nchi inayoweza peke yake kutatua janga la tabianchi akisema, “Huu ni wakati wa kila mtu kushiriki. Umoja wa Mataifa unajitolea kufanya kazi ili kujenga uaminifu, kutafuta ufumbuzi, na kuhamasisha ushirikiano ambao ulimwengu wetu unahitaji sana.”
Na kwa vijana, kwa mashirika ya kiraia, kwa miji, mikoa, biashara na wengine ambao wamekuwa wakiongoza hatua kuelekea ulimwengu salama na safi, Katibu Mkuu amesema, Asante. -
05 JUNI 2024
Hii leo jaridani tunaangazia siku ya mazingira duniani, na msaada wa kibinadamu nchini Haiti. Makala tunamulika hatua za kurejesha afya ya ardhi iliyoharibiwa na mashinani tunasalia hapa makao makuu kusikia ujumbe wa Martin Griffiths anayestaafu mwishoni mwa Juni.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres asubuhi ya leo saa za New York, Marekani kupitia Hotuba Maalumu kuhusu Hatua Dhidi ya Mabadiliko ya Tabianchi ametahadharisha kuhusu hatari ya wazi ya uwezekano wa ongezeko la joto juu ya nyuzijoto 1.5 za selsiasi linaloukabili ulimwengu ikiwa uzalishalishaji wa hewa chafuzi utaendelea kwa viwango vya sasa. Licha ya machafuko na mashambulizi yanayofanywa na makundi yenye silaha huko nchini Haiti, shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa chakula duniani limeendelea kuimarisha operesheni zake katika mji mkuu wa Port-au-Prince na kusaidia jamii zilizoathiriwa na ghasia ambapo kwa mwezi Mei shirika hilo limeweza kuwafikia zaidi ya watu 93,000.Katika makala ikiwa leo ni siku ya mazingira duniani Umoja wa Mataifa unaisa dunia kuchukua hatua sasa kurejesha afya ya ardhi iliyoharibiwa na kujenga mnepo dhidi ya kuongezeka kwa hali ya jangwa na ukame. Na hiyo ndio kaulimbiu ya siku ya mwaka.Mashinani tunasalia hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York kusikiliza ujumbe, wa Mratibu wa Umoja wa Mataifa wa Masuala ya Kibinadamu na Misaada ya Dharura Martin Griffiths anayestaafu wadhifa huo mwishoni mwa Juni.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu! -
WFP yafanikiwa kufikisha Msaada wa chakula nchini Haiti licha ya hali tete ya usalama
Licha ya machafuko na mashambulizi yanayofanywa na makundi yenye silaha huko nchini Haiti, shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa chakula duniani limeendelea kuimarisha operesheni zake katika mji mkuu wa Port-au-Prince na kusaidia jamii zilizoathiriwa na ghasia ambapo kwa mwezi Mei shirika hilo limeweza kuwafikia zaidi ya watu 93,000.
Kwa mujibu wa tathmini ya viwango vya njaa iliyofanyika mwezi Machi mwaka huu nchini Haiti, takriban watu milioni 5 ambao ni sawa na nusu na idadi ya watu wote wa taifa hilo, wanakabiliwa na ukosefu wa uhakika wa chakula ikiwemo watu milioni 1.64 ambao wametajwa kuwa hatua moja tu kabla ya kufikia baa la njaa yani IPC4.
Maisha ya wanajamii yamebadilika sana, wale waliokuwa wanaweza kujikimu sasa wamegeuka ombaomba kama anavyoeleza bibi Heugenie Pierre Charles, mwenye umri wa miaka 70 mkazi wa Port- au – Prince.
“Kuna wakati mwingine nakuwa na njaa sana. Nawaomba watu wanaokula wanigawie kidogo wanachokula. Lakini wananidhalilisha. Huko nyuma sikuwahi kuwa naomba, nilikuwa naweza kuendesha biashara zangu. Inaniuma sana. Nilikuwa na kazi yangu, lakini magenge ya wenye silaha yamesababisha nifunge. Na sasa naishi katika hali ambayo inanifanya nalia. Nipo hapa katika kambi ya wakimbizi wa ndani. Nilikuwa nimebakiwa na birika tu. Kwa bahati mbaya imeibiwa. Sasa sina kitu chochote. Nilikuwa natumia birika yangu kuchemsha chai na chakula.”
WFP kwa kutambua madhila yanayowakumba wananchi mwezi Mei ilifanikiwa kuingiza shehena ya chakula nchini Haiti na miongoni mwa walionufaika ni zaidi ya wananchi 93,000 walioko Cité Soleil, mojawapo ya vitongoji vilivyo vigumu kufikika kutokana na usalama, walifanikiwa kufikishwa msaada wa chakula kwani wananchi hao wako hatarini zaidi kukumbwa na njaa.
Mwakilishi wa WFP nchini Haiti Jean-Martin Bauer anasema ndege ya shirika hilo iliyotua Port au Prince mwezi Mei imekuwa mkombozi.
“Barabara za kuingia na kutoka katika mji wa wa Port-au-Prince zinashikiliwa na makundi yenye silaha. Bandari ilifungwa muda mrefu uliopita Kwani iliporwa, na uwanja wa ndege nao ukafungwa, kwa ufupi Port au Prince kwa miezi michache imekuwa kama kisiwa. Kwa hivyo ni muhimu sana kwa WFP na wasaidizi wengine wa kibinadamu kuweza kuleta misaada mjini hapa na, kuendesha programu muhimu. Kwa hivyo huduma muhimu ambazo watu wanategemea, iwe huduma ya afya, maji na usafi wa mazingira, chakula, zinahitaji usafirishaji wa bure wa bidhaa na watu, na hivi sasa hatujapata hiyo. Kwa hivyo tunachofanya na safari hii ya ndege ni kufungua tena mlango huo na kuhakikisha kuwa mahitaji muhimu yanaingia ili kuruhusu huduma hizi muhimu kufanya kazi.”
Mbali na kusambaza misaada mbalimbali ya chakula kwa mwaka huu WFP imesaidia zaidi ya watu 108,000 waliokimbia makazi yao kwa kuwapatia chakula cha moto. Pia wanatoa Msaada wa kuwapatia fedha taslimu na mwitikio huu wa kibinadamu pia unajumuisha nyongeza ya lishe kwa kaya zilizo na wajawazito au watoto walio chini ya umri wa miaka mitano.