Habari za UN - Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

  1. 11h ago

    19 JUNI 2026

    Hii leo jaridani tunaangazia wito wa UN wa kulinda mamilioni wa wakimbizi kote duniani, masuala ya kijinsia Zanzibar nchini Tanzania, na ripoti mpya ya Katibu Mkuu wa UN kuhusu watoto katika maeneo ya machafuko imeonesha hali ya kutisha duniani.Kuelekea maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wakimbizi kesho Juni 20, viongozi wa Umoja wa Mataifa wametoa wito wa kuimarishwa kwa mshikamano na hatua za kimataifa za kuwalinda mamilioni ya watu waliolazimika kuyakimbia makazi yao kote duniani kutokana na vita, vurugu na mateso.Ripoti mpya ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu watoto katika maeneo ya machafuko imeonesha hali ya kutisha duniani. Takribani watoto 24,174 waliuawa, kujeruhiwa, kulazimishwa kujiunga na makundi yenye silaha, kubakwa au kuathiriwa kwa namna nyingine na ukiukwaji mkubwa wa haki katika maeneo yenye mizozo mwaka 2025.Je, maisha yangekuwaje kama kila manusura wa ukatili wa kijinsia angejua mahali pa kupata msaada kwa wakati? Kisiwani Zanzibar nchini Tanzania Shirika la Umoja wa Mataifa la Masuala ya Wanawake (UN Women), kwa ufadhili wa Muungano wa Ulaya (EU) na kwa ushirikiano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, linaimarisha upatikanaji wa haki na huduma za msaada kwa manusura wa ukatili wa kijinsia, hususan katika maeneo ya pembezoni. Kupitia mradi wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Wasichana Zanzibar na Kuimarisha Uongozi wa Wanawake, manusura wanapata habari muhimu, ushauri nasaha na msaada wa kisheria wakati wowote.Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!

    10 min
  2. 1d ago

    18 JUNI 2026

    Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina. Katika mkutano wa 19 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Haki za Watu Wenye Ulemavu uliomalizika wiki iliyopita baadhi ya wahudhuriaji walikuja na wakalimani wao, kutoka Tanzania Mbunge Nassriya Nassir Ali mwenye ulemavu wa kusikia au Kiziwi aliambatana na mkalimani wake Tusajigwe Ernest. Baada ya mkutano huo Leah Mushi aliketi na Tusajigwe na hapa anaanza kwa kueleza kuhusu taaluma yake. Pia tunakuletea muhtasari wa habari.Kauli za chuki zinaendelea kuhatarisha mshikamano wa jamii na amani duniani, ameonya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres akisema mara nyingi ndizo chachu ya vurugu, migogoro na uhalifu mkubwa dhidi ya ubinadamu. Katika ujumbe wake wa Siku ya Kimataifa ya Kupambana na Kauli za Chuki, leo Juni 18, Guterres amesema makundi kama wanawake, wahamiaji, wakimbizi, watu wenye ulemavu na jamii ya LGBTQIA+ mara nyingi hulengwa na ujumbe wa chuki. “Kauli za chuki ndio hatua ya kwanza katika njia ya kuwanyima watu utu wao, njia ambayo mara nyingi hupelekea vurugu, migogoro na uhalifu wa kutisha.” Pia ameonya kuwa mitandao ya kijamii imeongeza kasi ya kusambaa kwa chuki duniani.Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa Kulinda Amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, MONUSCO, umetangaza kwa masikitiko hii leo kifo cha mfanyakazi wa kampuni iliyokuwa ikitoa huduma kwa ujumbe huo, aliyefariki dunia kutokana na Ebola mjini Bunia. MONUSCO imesema mfanyakazi huyo alikuwa ameacha kufanya kazi na ujumbe huo tangu Mei 22 mwaka huu na hakuwa amefika katika maeneo ya MONUSCO kwa zaidi ya siku 21 kabla ya ugonjwa huo kuthibitishwa. Ujumbe huo umetuma salamu za rambirambi kwa familia, ndugu, marafiki na wafanyakazi wenzake na marehemu.Na Shirika la Umoja wa Mataifa la Hali ya Hewa Duniani, WMO, limesema matukio mabaya ya hali ya hewa na mabadiliko ya tabianchi yaliathiri takriban watu milioni 13 barani Afrika mwaka 2025 na kusababisha vifo zaidi ya watu 3,000. Ripoti mpya ya shirika hilo iliyotolewa leo mjini Geneva Uswisi inaeleza kuwa mafuriko yalikuwa janga lililoripotiwa zaidi, huku yakisababisha hasara kubwa za kiuchumi na kibinadamu. WMO pia imeonya kuwa barafu katika maeneo ya milima ya Afrika, ikiwemo Mlima Kilimanjaro, inaendelea kutoweka kwa kasi, wakati kina cha bahari katika baadhi ya maeneo ya pwani kikipanda kwa kiwango kikubwa kuliko wastani wa dunia. WMO imesisitiza kuwa Afrika bado ina pengo kubwa katika mifumo ya tahadhari za mapema, ingawa maendeleo yanaendelea kufanyika.Mwenyeji wako ni Feissal Kirwa, karibu!

Ratings & Reviews

5
out of 5
5 Ratings

About

Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

More From United Nations